Sunday, March 9, 2014

Udhibiti sahihi wa visumbufu vya mimea ni njia ni njia mojawapo ya kuongeza tija katika kilimo, na ubora wa mazao. Kwa kuwa kwa kipindi hiki kuna aina za mbegu chotara nyingi za kahawa hasa zinazozalishwa na TaCRI zenye uvumilivu wa magonjwa sugu ya Chulebuni,CBD, na Kutu ya mjani. Mbegu hizi zinazaa sana na zina muonjo mzuri, changamoto kubwa imebaki kwenye udhibiti wa wadudu waharibifu. Hapa chini nitaelezea baadhi ya wadudu hao na jinsi ya kuwadhibiti.

1. KIMATIRA

Kimatira ni mdudu anayeshambulia kahawa aina ya Arabika. Madhara ya mdudu huyu ni kupunguza wingi wa na ubora wa kahawa. Wastani wa vimatira wawili au watatu kwa mti kwa eneo wanaweza kusababisha uharibifu wa zao kwa asilimia 45. Hufyonza matunda machanga na kusababisha kuoza. Hufyonza majani na machipukizi na kusababisha utoaji wa matawi madogo madogo na pingili fupi fupi. Dalili hizi zikionekana mkulima achunguze kuwepo kwa Kimatira kabla ya kuchukua hatua za kudhibiti. Hufyonza vikonyo vya maua na kusababisha kubadilika rangi kuwa nyeusi.

MADHARA YAKE.

. Husababisha kukauka kwa maua na kupukutika kwa matunda.

. Mashambulizi haya pia huingiza ugonjwa wa ukungu ambao huozesha kahawa na kuwa mapepe, hivyo hupunguza ubora na wingi wa mavuno.

NAMNA YA KUMDHIBITI KIMATIRA.

. Pogolea matawi mara kwa mara kadri inavyoshauriwa.
. Punguza kivuli cha miti na nigomba.
. Tumia Fenitrothion 50% EC millilita (cc) 25 za dawa kwa lita 15 za maji, Selecron 720% EC millilita (cc) 25 za dawa kwa lita 15 za maji.
. Hakikisha shamba lako linakuwa safi kila wakati ili kuzuia kuzaliana kwa mdudu huyu.
. Dhibiti wadudu hawa mara tu wanapoonekana wastani wa kimatira wawili au watatu kwa mti shambani mwako.
. Ni muhimu mashamba ya majirani yakadhibitiwa kwa wakati mmoja na shamba lako.

FAIDA ZA KUMDHIBITI KIMATIRA.

Mkulima akimdhibiti kimatira atapata faida zifuatazo;

. Atakuwa amepunguza kuzaliana kwa wadudu.
. Atakuwa ameongeza mavuno na ubora wa kahawa.
. Atakuwa amejiongezea kipato chake na kuwa maisha mazuri zaidi.
. Atakuwa ameongeza pato la taifa kwa ujumla.

2. BUNGUA MWEUPE (MAPEMBE).

Bungua mweupe au " Mapembe" ana mabawa yenye magamba meusi na kijivu. Pia ana kipapasi kirefu (antena). Wiki 1 hadi 2 baada ya mvua za vuli kuanza, mdudu huyu hutoka ndani ya shina la kahawa na kujilisha kwenye magamba machanga au matunda ya kahawa. Uharibifu wake wakati huu ni mdogo. Mdudu huyu hutaga mayai chini ya magamba kwenye shina la kahawa sentimita 30 kutoka usawa wa ardhi. Mayai huanguliwa baada ya wiki tatu na kuwa kiwavi ambaye huanza kujilisha kwa kuparua magamba ya kahawa kabla ya kutoboa na kuingia ndani ya mti ambapo hukaa kwa miaka miwili. Bila ya kumdhibiti mdudu huyu anaweza kusababisha hasara kwa kufyonza virutubisho na kufanya mti wa kahawa kuwa wa njano na baadaye kufa.

HATUA HATARI ZA MAPEMBE.

Hatua ya kiwavi cha mdudu huyu ndicho kinachosababisha madhara makubwa kwenye mti wa kahawa.

Dalili zake:
. Miti iliyoshambuliwa inakuwa na matundu kwenye mashina na hasa katika sehemu ya chini ambapo unga unga wa njano huonekana.
. Majani ya mti ulioshambuliwana kuathirika sana, hugeuka rangi ya njano na hatimae hunyauka na kufa.

Namna ya kumdhibiti:

. Njia muhimu ya kumdhibiti Mapembe ni kuutunza mti wa kahawa kuwa na afya nzuri kwa kupanda kwa nafasi iliyopendekezwa, kuweka mbolea ya kutosha, kuweka shamba katika hali ya usafi na kudhibiti wadudu na magonjwa.

. Baada ya kuvuna, kwangua magamba ya shina la kahawa (usawa wa goti toka ardhini) kwa kutumia gunzi la mahindi, ili kupunguza mazalia ya mdudu huyu, pia hufanya mayai na viwavi vyake kuonekana kwa urahisi na kushambuliwa na wadudu maadui wa mdudu huyu.

. Ua kiwavi wa bungua mweupe kwa kumchokonoa kwa waya ndani ya shimo.

. Vutia sisimizi watakao mla bungua kwa kuweka mafuta ya wanyama kwenye tundu.

. Kata miti iliyoshambuliwa sana (stumping), na kama lava amepekecha kuelekea chini, mtoe kwa waya.

. Paka chokaa, udongo au majivu ili kukausha mayai yasianguliwe kwenye shina na matawi.

. Nyunyiza mkojo wa ng'ombe uliovundikwa kwa siku 14 ili kuua au kufukuza wadudu hao.
. Kagua shamba na kamata na kuwaangamiza hasa mvua za vuli zinapoanza.

Mambo muhimu ya kuzingatia:

Ni muhimu mashamba ya jirani yakadhibitiwa kwa wakati mmoja ili kuzuia mapembe kuhamia mashamba hayo.

3. RUHUKA.

Ruhuka ni mdudu hatari ambaye huishi kwenye mibuni na mimea jamii ya mikunde, ambayo huwa ni mbadala wakati matunda ya kahawa hayapo. Mdudu huyu hushambulia zaidi mibuni aina ya Robusta na Arabica kwenye ukanda wa chini. Madhara ya mdudu huyu huendelea mpaka ghalani. Asipodhibitiwa anaweza kusababisha uharibifu wa zao shambani mpaka asilimia 90.

Dalili muhimu, uharibifu na madhara yake:

. Matunda mabichi au yaliyoiva huwa na tundu moja au zaidi kwenye kitovu cha tunda.

. Punje zilizoshambuliwa hubadilika rangi na kuwa kijani cha bluu. Katika hali hii viwavi huwepo ndani ya punje.

. Matundu yaliyotobolewa huweza kuwa njia ya kupenyeza ukungu na bacteria na kupunguza ubora wa zao.

. Ruhuka huendelea kushambulia punje ghalani na hivyo kushusha ubora wa kahawa.

Namna ya kumdhibiti Ruhuka:

. Epuka kuotesha miti ambayo inaficha hawa wadudu wakati usio msimu kama Lantana camara.

. Punguza kivuli cha shambani.

. Pogoa matawi inavyoshaushauriwa.

. Chuma kahawa mara kwa mara (kila baada ya siku 14) ili kahawa isikauke juu ya mti na hivyo kuzuia masalia ya matunda yenye Ruhuka.

. Okota matinda yote yaliyoanguka shambani wakati wote, na ondoa matunda yote yaliyobaki kwenye kahawa baada ya msimu. Chimba shimo na ufukie matunda hayo. Kwa kufanya hivyo unakatisha mzunguko wa maisha ya ndudu huyu.

. Weka matandazo ili kuendeleza wadudu marafiki wanaokula Ruhuka, hii pia husaidia kuozesha matunda yaliyodondoka chini.

. Chunguza kuwepo kwa Ruhuka katika miezi ya Februri na Machi. Akiwepo nyunyizia dawa za asili kama mwarobaini na utupa. Uchunguzi ukionyesha kuendelea kuwepo kwa Ruhuka, nyunyizia sumu za viwandani kama vile Thiodan 35EC au Dursban 48EC (15mls kwenye lita 20 za maji). Hii ifanyike kabla ya Ruhuka kuingia ndani ya punje.

. Tumia njia za kiasili kumdhibiti Ruhuka kwa mfano mtego wa chupa kwa kutumia kileo kama vile gongo, mbege, rubisi na konyagi.

. Hakikisha kwamba dawa inapigwa miezi 4 kabla ya kuvuna kahawa. Ni vyema mashamba ya majirani pia yadhibitiwe kwa wakati mmoja na shamba lako.

Faida za kumdhibiti Ruhuka:

. Kuongeza wingi wa kahawa.
. Kupunguza hasara na kuongeza kipato.
. Kupunguza uwezekano wa kupata sumu ya ukungu (OTA).

4. KIDOMOZI.

Kidomozi ni nondo mdogo mweupe ambaye mchana hujificha chini ya majani ya kahawa na kuruka usiku. Kidomozi hushambulia zaidi majani ha kahawa aina ya Arabika. Mashambulizi yanayofanywa na wadudu hawa hupunguza mazao kwa asilimia 8-10. Nondo wa kidomozi hutaga mayai juu ya majani ya kahawa na huangua viwavi wadogo ambao huharibu mjani kwa kuacha makovu ya kahawia.

Dalili zake:
. Majani yaliyoshambuliwa yanakuwa na mabaka ya rangi ya kahawia na juu ya jani linaonekana lina mabaka ya ukavu.

. Endapo ukifumua kovu kwa kutumia waya mwembamba utaona viwavi wembamba na weupe.

Madhara yake:

. Mashambulizi ya viwavi hawa hupunguza eneo la majani linalotengeneza chakula cha mmea na kusababisha majani kupukutika.

. Kupukutisha majani husababisha mti wa kahawa kushindwa kutengeneza chakula cha kutosha kujilisha na hasa kulisha matunda.

Namna ya kumdhibiti kidomozi:

. Zingatia usafi wa shamba (kukata matawi, kukatua shamba na kuweka matandazo).

. Punguza kivuli shambani ili mwanga wa jua upenye kwa asilimia 60.

. Tumia dawa ya asili kama mkojo wa ng'ombe kwa uwiano wa 1:4 (mkojo:maji) kwa kunyunyizia kwenye shamba la kahawa.

. Tumia Selecron 720EC cc 25 za dawa kwenye lita 15 za maji, Dursban 48%EC tumia cc 30 za dawa kwa lita 15 za maji. Decis (Deltamethrin) 2.5%EC tumia cc 6.5 kwa lita 15 za maji, Furadan 5G (Carbofuran) tumia gram 30 kwa mti kila mwanzoni mwa mvua (Dawa hii ya carbofuran iwekwe chini kwenye mizizi).

. Dawa hizi zitumike wakati nondo 30 au zaidi wanapoonekana kwenye mti.
. Tumia dawa hizi baada ya wiki moja nondo wa mdudu huyu wanapokuwa wengi. Rudia tena kupiga dawa baada ya wiki 2 hadi 3.

. Badilisha dawa za kudhibiti mara kwa mara kwani utumiaji wa aina moja ya dawa husababisha wadudu hawa kuwa sugu.

Faida za kumdhibiti kidomozi:

Mkulima akidhibiti kidomozi atapata faida zifuatazo:
. Atakuwa amepunguza kuzaliana kwa wadudu hawa
. Atakuwa ameongeza wingi wa mavuno na ubora wa kahawa.
. Atakuwa amejongezea kipato chake na kuwa na maisha mazuri zaidi.
. Atakuwa ameongeza pati la taifa kwa ujumla.

6. UWIWI.

Ni mdudu msumbufu wa maeneo ya nyanda za chini kwa hapa kwetu Tanzania. Hushambulia matunda na kuyachubua huku akifungamanisha matunda kadhaa kwa utando wa kahawia. Matunda hutobolewa na kukaushwa. Huweza pia kutoboa na kuharibu sehemu za juu zinazokua za matawi.

Kumdhibiti:
. Usafi wa shamba.
. Kukata matawi.
. Kuokota na kufukia matunda yaliyoharibiwa na yaliyofungamanishwa.
. Kuweka matandazo.
. Madawa yafaayo ni sawa na yale yaliyoainishwa kwa udhibiti wa kidomozi hapo juu.

7. BUNGUA NJANO.

Hushambulia majani hadi shina na kuathiri usafirishaji wa virutubisho, afya ya mti pamoja na mavuno. Dalili zake ni kunyauka sehemu za juu za matawi, matundu mengi madogo madogo kwenye tawi, matawi kuwa dhaifu na kuvunjika hasa kama yamezaa sana.

Kumdhibiti:
. Usafi wa shamba.
. Kuondoa matawi yaliyoathirika na kuyachoma au kuyafukia.
. Kuchokonoa matundu ya chini.
. Dawa asilia kama Utupa na Mwarobaini, na za viwandani kama Ultracide na Decis.

8. VITHIRIPI.

Hawa huweza kuwa tishio wakati wa ukame wa muda mrefu. Hushambulia sehemu zote laini za mmea (majani, vitawi vichanga na matunda) kwa kufyonza chembechembe hai. Majani yaliyoathirika yana rangi ya shaba juu na chini.

Kuwadhibiti:
. Usafi wa shamba.
. Kuweka matandazo, kivuli na kumwagilia maji ipasavyo.
. Piga dawa pale tu ukiona vithiripi watatu kwa jani. Waweza kutumia Selecron 50EC, millilita 50 kwa lita 15 za maji, utupa au mwarobaini.

Makala hii nimeiandaa kwa msaada wa kitaalam zaidi kutoka katika Taasisi ya uendelezaji na uboreshaji wa zao la kahawa Tanzania (TaCRI), kituo cha Mbimba- Mbozi, Mbeya.

Ahsanteni sana!

Imetayarishwa na kuandikwa na Marcodenis E. Misungwi- Agriculture Extension Field Officer at Mbozi District, Mbeya.

1 comments:

  1. I wanna say thanks to DARK WEB for helping me boost my credit score from 420 to 840 excellent. Last year June i wasn't able to afford to pay my house rent due to my low credit score until i met dark web he help me erased all bad reports on my credit line, boost my credit score. I would advise y'all to get in touch with him if you have any issues with your credit score, just text him on his email; DARKWEBONLINEHACKERS@GMAIL.COM or his number (803) 392-1735

    ReplyDelete