Monday, March 10, 2014

Kahawa ni zao kubwa la biashara linaloliingizia taifa fedha nyingi za kigeni. Ni la pili baada ya Tumbaku. Lakini zao hili linakabiliwa na changamoto nyingi ambazo ni magonjwa na wadudu achilia mbali Pembejeo, haya yote yanamuhusisha moja kwa moja mkulima. Makala yangu iliyopita nilijadili kwa kina Wadudu wasumbufu kwenye kahawa na jinsi ya kujaniliana nao.

Leo nitaongelea magonjwa sugu ya kahawa na udhibiti wake.

1. CHULEBUNI (CBD).

Chulebuni ama kama ujulikanavyo kama Coffee Berry Disease (CBD), ni ugonjwa mbaya sana na huenea kwa kasi. Mbuni ulioshambuliwa haufi ila mkulima anaweza kupoteza mpaka asilimia 90 ya mavuno kama hatazingatia namna bora ya kuuzuia. CBD huathiri matunda ya kahawa hasa kanda za juu na kati. Ushambuliaji ni mkubwa zaidi wakati wa masika kwani CBD hupenda hali ya unyevu na hali ya baridi.

Dalili na madhara ya CBD:

* CBD hushambulia mibuni katika hatua tatu muhimu ambazo ni:
. Maua yanapochanua.
. Punje zikiwa changa na laini.
. Punje zinazoiva.

* Madhara makubwa hutokea walati punje zikiwa changa na laini amnapo:
. Maua yaliyoshambuliwa hunyauka na kuanguka.
. Vidonda vyeusi na vilivyobonyea huonekana kwenye matunda yaliyoshambuliwa. Mengi huoza na kudondoka. Yaliyobakia hukaukia kwenye mti na kuwa chanzo cha uambukizaji kwenye mavuno ya msimu unaofuata.

* Matunda yaliyoiva hukaukia kwenye matawi na huvunwa kama buni.

* Hupunguza zao kwa asilimia kati ya 30 na asilimia 60 wakati mwingine hufikia hadi asilimia 90.

* Kudhibiti CBD hufikia hadi asilimia 35 ya gharama za uzalishaji.

* Hupunguza ubora wa kahawa kwa kiasi kikubwa.

Jinsi ya kuzuia chulebuni (CBD):
- Panda aina mpya ya kahawa inayohimili mahambulizi ya Chulebuni ambayo ni mkombozi dhidi ya ugonjwa huu hatari.
- Punguza kivuli shambani.
-Kata matawi kwa wakati na sahihi. Ondoa maotea mara kwa mara.
- Ondoa masalia ya buni zilizoathirika na teketeza kwa moto.
- Kwangua magamba kwenye mashina machafu ya kahawa.
- Anza kunyunyizia vizuia kuvu kukinga matunda machanga ndani ya wiki tatu kabla ya mvua za msimu kuanza.
- Hamasisha majirani kuzuia chulebuni kwa wakati mmoja.

2. KUTU YA MAJANI (LEAF RUST).

Kutu ya majani ni ugonjwa unaoathiri majani ya kahawa hasa kanda za chini na kati. Ugonjwa huu unaathiri kahawa aina zote; Robusta na Arabika. Kutu ya mjani isipodhibitiwa inaweza kupunguza mavuno kwa asilimia 60.

Dalili za ugonjwa:

Majani yaliyoshambuliwa hutokeza madoa madoa ya manjano chini ya jani

Madhara yake:
. Kutu ya majani hupunguza eneo la jani la kutengeneza chakula. Pia hudababisha kupukutika kwa majani yanayolisha matunda na kukuza mmea.
. Kwa hali hiyo husababisha madhara ya mmea kutoa punje ndogo zenye ubora hafifu.
. Ugonjwa ukishamiri hukausha matawi, shina zima na hatimaye mti mzima kufa.

Hali zinazochangia kuenea kwa kutu ya majani:
- Unyevu wa hewani unapokuwa zaidi ya aslimia 80 na unapoambatana na kivuli cha kupita kiasi kwenye shamba.
- Msongamano wa machipukizi na matawi katika mti wa kahawa.

Jinsi ya kudhibiti ugonjwa wa kutu ya majani:
- Punguza kivuli kuzunguka mti wa kahawa.
- Pogolea machipukizi na matawi katika mti wa kahawa.

Kuzuia kutu ya majani:
i) Panda aina mpya zinazovumilia magonjwa ya kutu ya majani na chulebuni.
ii) Boresha huduma muhimu ikiwa ni pamoja na lishe ili kuongeza uvumilivu wa magonjwa hususani ugonjwa wa kutu ya majani.
iii) Tumia viua kuvu kwa wakati na vipimo sahihi. Unyunyiziaji wa kwanza ufanywe ndani ya wiki tatu kabla ya mvua kunyesha, na kuendelea hadi mara tatu mpaka nne kwa msimu.
iv) Shirikisha na majirani kudhibiti kutu ya majani.

MAGONJWA MENGINE YA KAHAWA.

Yapo magonjwa mengine kadhaa ya kahawa ambayo umuhimu wake umemezwa na magonjwa mawili niliyozungumzia hapo juu. Ningependa kuyataja tu baadhi yake pamoja na mbinu za kuyazuia au kuyatibu.

3. BAKAJANI (Brown eye spot).

Ugonjwa huu huenezwa na kimelea aitwaye "Cercospora cofficola". Hudhibitiwa kwa utunzaji bora wa shamba na kutumia morututu.

4. UGONJWA WA PUNJE ( Bean disease).

Huu huambukizwa na kuvu aitwaye "Nematospora coryli" akienezwa na kimatira. Ili kuepukana na ugonjwa huu, ni lazima kuchukua hatua za kumdhibiti kimatira.

5. UGONJWA WA MASHINA (Scarly bark disease).

Ugonjwa huu hujulikana kama "Ukungu" kwa wakulima walio wengi, upo wa aina mbili ambao wakulima huwa wanashindwa kutofautisha na huuita kwa ujumla wake Ukungu. Aina hii ya kwanza ya ukungu huambukizwa na kuvu aitwaye "Fusarium lateritium". Hakuna udhibiti wa kitaalam mpaka sasa ila kung'oa mti mzima na kupanda upya. Ukishang'oa choma mti hapohapo na acha kwa muda angalau hata misimu miwili au mitatu kisha panda upya.

6. UGONJWA WA KUOZA MIZIZI (Root rot disease).

Huu ugonjwa unafanana kabisa na ugonjwa wa mashina, ni ukungu wa aina ya pili kama unavyojulikana na wakulima wengi. Huambukizwa na kuvu aitwaye "Armillaria mellea". Hakuna udhibiti ila kung'oa na kupanda upya baada ya muda wa misimu miwili au mitatu hivi.

Ndugu zangu wakulima, wataalam na wadau wote wa kilimo, hakikisheni mnajitahidi kwa kadri inavyowezekana kudhibiti magonjwa hayo. Kwa kufanya hivyo kutanuongezea mkulima kipato chake na pato la taifa kwa ujumla.

Ahsanteni sana!

Imetayarishwa na kuandikwa na Marcodenis E. Misungwi, Agriculture Field Extension Officer.

1 comments:

  1. CONTACT: onlineghosthacker247 @gmail. com
    -Find Out If Your Husband/Wife or Boyfriend/Girlfriend Is Cheating On You
    -Let them Help You Hack Any Website Or Database
    -Hack Into Any University Portal; To Change Your Grades Or Upgrade Any Personal Information/Examination Questions
    -Hack Email; Mobile Phones; Whatsapp; Text Messages; Call Logs; Facebook And Other Social Media Accounts
    -And All Related Services
    - let them help you in recovery any lost fund scam from you
    onlineghosthacker Will Get The Job Done For You
    onlineghosthacker247 @gmail. com
    TESTED AND TRUSTED!

    ReplyDelete